Wimbi jipya la mashambulizi ya chuki dhidi ya wageni, linalowalenga wahamiaji wa Kiafrika na biashara zao huko Afrika Kusini linatishia kuteteresha uhusiano wa nchi hiyo na nchi nyingine za Afrika.Katika siku za hivi karibuni makundi ya watu waliokuwa na mapanga, marungu na mikuki waliwashambulia raia wa kigeni katika mitaa ya miji ya Johannesburg na Cape Town wakiwatuhumu kuwa wanatumia fursa za kazi na ajira wa wazawa.Nigeria imemwita balozi wa Afrika Kusini kupinga ongezeka la mashambulizi ya chuki dhidi ya wageni (xenophobia) nchini humo, hatua inayoonyesha kuongezeka mvutano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.Haya yanakuja wakati ambapo Afrika Kusini, uchumi mkubwa zaidi wa viwanda barani Afrika, inakabiliwa na mashinikizo ya kijamii yanayoongezeka kutokana na ukosefu wa ajira wa karibu 30%, jambo ambalo limechangia kuongezeka chuki dhidi ya wahamiaji na katika baadhi ya matukio, vurugu na machafuko.Nigeria si nchi peke yake iliyojitokeza kuelezea wasiwasi wake kuhusu hujuma na mashambulizi yanayolenga raia wa kigeni nchini Afrika kusini; bali kabla ya hapo Ghana na Zimbabwe zilikuwa zimewasilisha malalamiko kuhusu matukio ya “chuki dhidi ya wageni”, jambo linaloashiria kuongezeka mvutano wa kidiplomasia wa nchi za Afrika na Afrika Kusini.Serikali ya Ghana ilionya kuhusu hali ya usalama isiyotabirika huko Afrika Kusini, ikisema baadhi ya wageni walikuwa wameshauriwa kubaki katika makazi yao ili kuepuka mashambulizi yanayoweza kutokea.Takwimu rasmi zinaonyesha kuwa idadi ya raia wa kigeni nchini Afrika Kusini inazidi milioni tatu, ikiwa ni takriban asilimia 5.1 ya idadi ya watu. Wengi kati ya wageni hao wanatoka nchi jirani ndani ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).Kwa upande wake, serikali ya Afrika Kusini imelaani vurugu hizo zinazowalenga raia wa kigeni, ikisema kwamba mashambulizi dhidi ya wageni ni kinyume cha katiba na maadili ya kitaifa, na kusisitiza kwamba haitavumilia aina yoyote ya chuki, vitisho, au uporaji.