KHARTOUM, May 5, 2026 — Serikali ya Sudan imezituhumu Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Ethiopia kuhusika na shambulio la ndege zisizo na rubani (drones) lililolenga Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Khartoum, msemaji wa serikali alisema Jumanne, katika hatua inayoongeza mvutano wa kikanda.
Tuhuma hizo zimeibuka kufuatia mfululizo wa mashambulizi ya angani yaliyotokea Jumatatu, yaliyolenga uwanja mkuu wa ndege wa mji mkuu huo pamoja na maeneo ya makazi na vituo kadhaa vya kijeshi.
Miongoni mwa maeneo yaliyoshambuliwa ni pamoja na kambi ya Signal Corps iliyoko Kaskazini mwa Khartoum na kituo cha mafunzo cha al-Markhiyat mjini Omdurman.
Akizungumza katika mkutano wa pamoja na waandishi wa habari mapema Jumanne, Waziri wa Mambo ya Nje wa Sudan Mohieddin Salem pamoja na msemaji wa jeshi Asim Awad Abd al-Wahab walisema kuwa wana “ushahidi wa moja kwa moja” unaoonyesha kuwa ndege hizo zisizo na rubani zilirushwa kutoka uwanja wa ndege wa Bahir Dar nchini Ethiopia.