Serikali ya Marekani imetangaza kuuawa kwa NiƱo Guerrero, anayedaiwa kuwa kiongozi wa kundi la uhalifu la Tren de Aragua, kufuatia operesheni ya kijeshi iliyofanywa nchini Venezuela.

Katika taarifa yake, Rais wa Marekani Donald Trump alisema operesheni hiyo ilitekelezwa kwa maagizo yake na kufanywa na Kamandi ya Kusini ya Jeshi la Marekani. Kwa mujibu wa taarifa hiyo, shambulio hilo lilikuwa la haraka na lililolenga kumuondoa Guerrero, ambaye ametajwa kuwa kiongozi wa kundi hilo linalohusishwa na uhalifu wa kimataifa.

Rais Trump alieleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za serikali yake kupambana na makundi ya uhalifu na yale yanayohusishwa na ugaidi. Pia alirejea ahadi alizotoa wakati wa kampeni yake kuhusu kuchukua hatua kali dhidi ya wahalifu wanaoingia nchini Marekani kinyume cha sheria.

Taarifa hiyo pia ilisema kuwa serikali ya Marekani ilishawahi kulitangaza kundi la Tren de Aragua kama shirika la kigaidi la kigeni na imekuwa ikiendesha operesheni mbalimbali dhidi ya magenge ya uhalifu na biashara ya dawa za kulevya.

Kwa mujibu wa Ikulu ya Marekani, operesheni hiyo iliratibiwa kwa karibu na mamlaka nchini Venezuela. Serikali ya Marekani imesisitiza kuwa itaendelea kuwafuatilia na kuchukua hatua dhidi ya viongozi na wanachama wa makundi ya uhalifu popote walipo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *