Liverpool, Uingereza — Klabu ya Liverpool imethibitisha rasmi kuondoka kwa meneja wake, Arne Slot, kufuatia msimu wa 2025/26 uliomalizika bila kufikia matarajio ya klabu na mashabiki.
Slot, raia wa Uholanzi, alikumbana na changamoto katika msimu wake wa pili akiwa Anfield, ambapo matokeo ya timu yalishuka na Liverpool kumaliza ligi katika nafasi ya tano, tofauti na mafanikio ya awali ya kutwaa taji la Ligi Kuu ya England (Premier League).
Katika taarifa yake, Liverpool ilieleza kuwa uamuzi wa kuachana na Slot haukuwa mwepesi. Klabu ilisisitiza kuwa mchango wa kocha huyo katika kipindi alichokuwepo umekuwa “mkubwa na wenye maana,” ikiutaja kuwa umeleta mafanikio kwa ujumla, sambamba na maadili ya kazi, bidii na kiwango cha utaalamu.
“Kuanzia mara ya kwanza tulipokutana naye, ilikuwa wazi kuwa ni mtu anayekubali na kukumbatia wajibu,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo, ikitaja uongozi wake wakati wa kipindi cha mafanikio na pia katika msimu uliopita alipokabiliwa na changamoto nyingi.
Liverpool iliongeza kuwa baada ya tathmini ya pamoja, klabu imefikia hitimisho kwamba mabadiliko ni muhimu ili kuendeleza maendeleo na kuhakikisha timu inaendelea kusonga mbele, ikisisitiza tena kuwa uamuzi huo ulifikiwa baada ya tafakari ya kina.
Klabu haikutangaza mara moja mrithi wa Slot, na taarifa zaidi kuhusu mipango ya benchi la ufundi zinatarajiwa kutolewa baadaye.