Mchambuzi wa masuala ya kimataifa Paul Musgrave ameandika katika jarida la Foreign Policy akidai kuwa kushindwa kwa Marekani katika vita vya karibuni dhidi ya Iran ni “janga la kimkakati” linalozidi hata athari za kushindwa kwa Marekani katika Vita vya Vietnam.
Kwa mujibu wa Musgrave, ingawa Vita vya Vietnam vilisababisha vifo vya wanajeshi wa Marekani karibu 60,000 ikilinganishwa na chini ya 20 katika vita dhidi ya Iran, athari za muda mrefu za kisiasa na kijiografia katika mgogoro wa Iran ni kubwa zaidi.
Anasema kuwa licha ya Vietnam kuacha doa katika historia ya Marekani, vita hivyo havikubadili kwa kiasi kikubwa malengo mapana ya kimkakati ya taifa hilo. Hata hivyo, kushindwa kwa sasa dhidi ya Iran kumeiacha Marekani ikiwa katika nafasi dhaifu zaidi huku baadhi ya malengo yake muhimu ya kimkakati yakipata pigo.
Musgrave anaeleza kuwa licha ya ubora wa kiteknolojia wa silaha za Marekani, vita hivyo vimeonyesha udhaifu katika akiba ya silaha za nchi hiyo na mipaka ya suluhu za kijeshi pekee. Badala ya kuunda serikali rafiki inayoweza kushawishika mjini Tehran, anasema vita hivyo vimeimarisha zaidi msimamo mkali wa Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC).
Aidha, vikosi vya Iran vilionyesha uwezo wa kupenya mifumo ya ulinzi ya Marekani. Picha iliyobaki akilini mwa wengi, anasema Musgrave, ni ile ya mabegi ya shule yaliyojaa damu ya wasichana wa Iran waliouawa katika shambulio la shule ya Minab.
Tofauti nyingine muhimu, kwa mujibu wa mchambuzi huyo, ni kwamba Marekani haiwezi kujiondoa kirahisi katika eneo hilo kama ilivyofanya Kusini Mashariki mwa Asia baada ya Vita vya Vietnam. Uchumi wa dunia sasa unategemea kwa kiasi kikubwa minyororo ya usambazaji kutoka Ghuba ya Uajemi kwa bidhaa muhimu kama vile nishati ya mafuta na gesi, heliamu, mbolea na alumini.
Musgrave anaonya kuwa uwezekano wa kuifanya Mlango wa Bahari wa Hormuz kuwa silaha ya kisiasa unaweza kusababisha madhara makubwa kwa biashara ya dunia, na pia kuashiria kushindwa kwa lengo la msingi la Marekani la kuhakikisha uhuru wa usafiri wa majini — sera ambayo imekuwepo kwa zaidi ya karne mbili.
Kwa ujumla, Musgrave anahitimisha kuwa vita hivi, ambavyo anaviita “vita vya hiari,” vimepunguza ushawishi wa Marekani duniani, huku washirika wake wakipoteza imani na wapinzani wake wakihamasika zaidi kupinga mamlaka ya Washington.