WASHINGTON — Mwanaume aliyedai kuwa mfanyabiashara kutoka Hong Kong anaripotiwa kumkaribia msaidizi wa bunge la Marekani kwa lengo la kupata taarifa za siri kuhusu sera ya Marekani dhidi ya China, katika tukio linaloonyesha mbinu zinazodaiwa kutumiwa na Beijing kukusanya taarifa nyeti nchini humo.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, mtu huyo aliyejitambulisha kama Chris Chen alimpa mfanyakazi wa Kamati ya Baraza la Wawakilishi inayoshughulikia masuala ya Chama cha Kikomunisti cha China ofa ya zaidi ya dola 10,000 za Marekani. Malipo hayo yalikuwa yakilenga kupata taarifa za mara kwa mara kuhusu shughuli za kamati pamoja na mjadala wa sera mbalimbali za Marekani.Ripoti zinaeleza kuwa Chen alipendekeza kuwepo kwa “kipindi cha majaribio” cha miezi mitatu, akiahidi kutoa dola 2,000 kama malipo ya awali kabla ya kuendelea na ushirikiano wa muda mrefu. Hata hivyo, msaidizi huyo alitoa taarifa kwa viongozi wake mara moja, jambo lililosababisha uchunguzi zaidi kuhusu utambulisho wa mtu huyo.
Kamati hiyo inaamini kuwa huenda mwanaume huyo alikuwa akihusishwa na vyombo vya ujasusi vya China badala ya kuwa mshauri wa biashara kutoka Singapore kama alivyodai.
Wachambuzi wa masuala ya usalama wanasema mbinu kama hizi zimekuwa zikihusishwa na juhudi za China kupata taarifa kuhusu biashara, teknolojia, usalama na sera za nje za Marekani.
Aidha, visa vya aina hiyo vimeendelea kuongeza wasiwasi kuhusu ushindani wa kiintelijensia kati ya Washington na Beijing.
Maafisa wa Marekani wameendelea kuonya kuhusu ongezeko la shughuli za ujasusi zinazolenga taasisi za serikali, huku wakisisitiza umuhimu wa tahadhari na usalama wa taarifa nyeti.