Brussels — Mamlaka ya Vyama vya Kisiasa na Taasisi za Umoja wa Ulaya imeanzisha rasmi mchakato wa uchunguzi dhidi ya chama cha siasa kali za mrengo wa kulia cha Europe of Sovereign Nations (ESN), hatua ambayo inaweza kukinyang’anya hadhi yake ya chama rasmi cha kisiasa cha Umoja wa Ulaya pamoja na ufadhili wa kifedha.
Kwa mujibu wa taarifa ya POLITICO, chama hicho kilichoanzishwa na chama cha AfD cha Ujerumani kinakabiliwa na tuhuma za kukiuka maadili ya msingi ya Umoja wa Ulaya.
Mamlaka hiyo imesema imepokea ushahidi unaohusisha matamshi ya kupinga wahamiaji, chuki dhidi ya Wayahudi, na kauli za kupinga haki za watu wa LGBT kutoka kwa baadhi ya vyama wanachama wa muungano huo. Aidha, ripoti ya kurasa 300 imetaja pia madai ya misimamo mikali ya kisiasa pamoja na uhusiano unaodaiwa kuwepo kati ya baadhi ya wahusika na chama cha United Russia.
Ripoti hiyo imejengwa juu ya rejea za maamuzi ya mahakama, machapisho ya mitandao ya kijamii, pamoja na taarifa za kijasusi. Miongoni mwa hoja zilizotajwa ni pamoja na hatua ya Ujerumani ya mwaka 2025 ya kukitambua chama cha AfD kama taasisi yenye msimamo mkali wa mrengo wa kulia.
Muungano wa ESN unahusisha vyama vya kitaifa kutoka nchi mbalimbali za Ulaya ikiwemo Ujerumani, Ufaransa, Poland, Bulgaria, Hungaria, Uholanzi, Slovakia, na Czechia. Muungano huo unatarajiwa kupokea zaidi ya euro milioni 2 kama ruzuku kutoka Umoja wa Ulaya mwaka 2026.
Iwapo mchakato huo utafanikiwa, ESN itapoteza ufadhili wake wa Umoja wa Ulaya na kutambuliwa kwake kisheria kama chama cha kisiasa cha EU. Hata hivyo, kundi lake ndani ya Bunge la Ulaya pamoja na wabunge wake 27 wa Bunge la Ulaya wataendelea kubaki.