Makamu wa Rais wa Marekani, JD Vance, amesema mazungumzo kati ya Marekani na Iran yamepiga hatua kubwa, huku pande hizo mbili zikiendelea kujadiliana kuhusu baadhi ya vipengele vya lugha ya makubaliano na vifungu vya rasimu ya mkataba unaotarajiwa kufikiwa.

Vance amesema bado ni vigumu kusema kwa uhakika ni lini au iwapo Rais Donald Trump atasaini hati ya makubaliano (MoU), akieleza kuwa bado kuna mjadala unaoendelea kuhusu baadhi ya vipengele vya maandishi ya makubaliano hayo. Hata hivyo, amesisitiza kuwa maendeleo yaliyofikiwa hadi sasa yanaashiria kuwa pande hizo zinakaribia kufikia hatua ya kuketi pamoja na kutatua masuala yaliyosalia.

Kwa mujibu wa Vance, Iran inaonesha nia ya kufikia makubaliano na pia kutaka kufunguliwa kwa Mlango-Bahari wa Hormuz, jambo ambalo Marekani nayo inaliona kuwa la muhimu. Ameeleza kuwa mazungumzo kati ya pande hizo mbili yanaendelea kuhusu suala hilo, huku Washington ikiamini kuwa Tehran imekuwa ikijadiliana kwa nia njema, angalau kwa hatua ya sasa.

Katika hatua nyingine, Vance amesema Iran imekubali kutotengeneza wala kutomiliki mpango wa nyuklia, na kwamba suala hilo litafuatiliwa na kuthibitishwa kadri muda unavyokwenda. Ameongeza kuwa hali ya sasa inaipa Marekani na washirika wake nafasi ya kuudhoofisha kwa kiasi kikubwa na kwa muda mrefu mpango wa nyuklia wa Iran.

Licha ya ishara hizo za matumaini, Vance amesema bado kunahitajika maendeleo ya ziada ili kufikia mwafaka wa mwisho, lakini akaonyesha matumaini kuwa mazungumzo yataendelea kuzaa matunda katika siku zijazo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *