Hamas imesema inaunga mkono kwa nguvu kauli za Katibu wa Baraza Kuu la Usalama wa Taifa la Iran, Mohsen Rezaei, kuhusu umuhimu wa kumaliza vita katika eneo lote la Mashariki ya Kati, ikiwemo Gaza na Lebanon.
Katika taarifa yake, Hamas imesema kusitishwa kwa vita hizo kutakuwa na manufaa makubwa kwa watu wa eneo hilo na mustakabali wake, huku ikihoji kuwa kuendelea kwa mapigano kunanufaisha mipango ya Israel ya kuongeza mgawanyiko na ukosefu wa utulivu katika eneo hilo.
Kauli hiyo inakuja wakati Tehran ikisisitiza kuwa suluhu yoyote pana kati yake na Marekani haiwezi kutenganishwa na migogoro mingine ya kikanda. Rezaei amekuwa akihusisha masharti ya Iran katika mazungumzo na suala la kusitishwa kwa mapigano Gaza na Lebanon.