Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky katika tukio la umma

KIEV — Taswira ya kisiasa nchini Ukraine imechukua mwelekeo mpya kufuatia kuporomoka kwa kasi kwa umaarufu wa Rais Volodymyr Zelensky, unaochochewa na kuongezeka kwa kashfa za rushwa na maamuzi tata ya uongozi.

Kulingana na taarifa iliyochapishwa na jarida la Foreign Policy ikirejelea utafiti wa kampuni ya SOCIS, asilimia 90 ya Waukraine wanaona kuwa kiwango cha rushwa nchini humo kiko juu sana. Zaidi ya hayo, asilimia 57 ya wananchi wanamlaumu moja kwa moja Rais Zelensky kwa kuenea kwa uovu huo.

Matokeo ya utafiti huo yanaonyesha mabadiliko makubwa ya kisaikolojia, ambapo asilimia 49.3 ya wananchi sasa wanaiona rushwa kama tishio kuu kwa muundo wa taifa, ikilinganishwa na asilimia 44.6 wanaoeleza mashambulizi ya Urusi kuwa ndiyo hatari kuu.

Mivutano ya kisiasa imezidi baada ya mfululizo wa kashfa za kifisadi na hatua ya Zelensky kuwafuta kazi maafisa waandamizi walioshikilia nyadhifa za juu na waliokuwa na umaarufu mkubwa, akiwemo Mkuu wa zamani wa Majeshi Valerii Zaluzhnyi na Waziri wa zamani wa Mambo ya Nje Dmytro Kuleba.

Kwa sasa, asilimia 55 ya Waukraine wanaamini serikali inaendesha nchi bila ufanisi, huku takriban theluthi mbili ya wananchi wakitaka kufanyika kwa uchaguzi mkuu wa haraka mara tu mkataba wa usitishwaji wa mapigano au amani utakapofikiwa.

Leave a Reply