WASHINGTON, MAREKANI

Shinikizo la kisheria limeongezeka dhidi ya Wizara ya Sheria ya Marekani kufuatia agizo jipya la mahakama linalotaka kuwekwa wazi kwa nyaraka nyeti zinazohusiana na mfanyabiashara marehemu Jeffrey Epstein, huku kukiwa na tuhuma nzito zinazomhusisha Rais wa Marekani, Donald Trump.

Jaji wa Shirikisho nchini humo, Emmet Sullivan, ametoa uamuzi mkali akibainisha kuwa Kaimu Mwanasheria Mkuu, Todd Blanche, amekiuka “Sheria ya Uwazi wa Nyaraka za Epstein” (Epstein Document Transparency Act). Katika uamuzi huo, Jaji Sullivan ameeleza kuwa upande wa utetezi umekiri kuwepo kwa ukiukwaji huo katika utekelezaji wa sheria hiyo inayolenga kuleta uwazi wa kashfa hizo za unyanyasaji wa kingono.

Kufuatia hatua hiyo, mahakama imeipa Wizara ya Sheria hadi kufikia tarehe 2 Julai kutoa maelezo ya kina. Wizara hiyo inatakiwa ama kuondoa vizuizi (censorship) na kuchapisha nyaraka hizo kikamilifu, au kutoa sababu madhubuti za kisheria zinazozuia nyaraka hizo kubaki kuwa siri.

Nyaraka hizo zinazovuta hisia za wengi zinatajwa kuwa na maelezo ya mshtuko. Sehemu ya nyaraka hizo inajumuisha kumbukumbu za mahojiano ya shirika la upelelezi la FBI na mwanamke mmoja, ambaye anadai kuwa akiwa na umri wa miaka 13 pekee, alitambulishwa kwa Donald Trump na Jeffrey Epstein na kisha kufanyiwa vitendo vya kikatili.

Aidha, jalada hilo lina shehena ya barua pepe za Epstein zinazozungumzia kile kinachoitwa “video za mateso” na shughuli za kingono zilizohusisha watoto walio chini ya umri wa kisheria. Vilevile, nyaraka hizo zinatarajiwa kuumbua majina ya watu wanaodhaniwa kuwa washirika wa Epstein, pamoja na rasimu za hati za mashtaka ambazo hazikuwahi kufikishwa mahakamani.

Hatua hii inatajwa kuwa pigo lingine kwa upande wa Trump na Wizara ya Sheria, huku ulimwengu ukisubiri kwa hamu kuona ikiwa siri hizo nzito zitawekwa hadharani ifikapo tarehe iliyopangwa na mahakama.

Leave a Reply