Waziri wa Ulinzi wa Israel Israel Katz amesema Israel itaendelea kuchukua hatua za kijeshi kulinda maeneo yake na kuzuia nchi nyingine, ikiwemo Uturuki, kuanzisha uwepo wa kijeshi ndani ya Syria.
Akizungumza akiwa katika eneo la Mlima Hermon katika eneo la Syria linalokaliwa kimabavu na Israel, Katz alisema kutoka eneo hilo Israel inaweza kuona maeneo ya Bonde la Bekaa nchini Lebanon, harakati za Hezbollah na mji wa Damascus.
Katz amesema:
“Rais wa Syria anapoamka asubuhi na kuona Mlima Hermon na kuona Jeshi la Ulinzi la Israel, lazima akumbuke kwamba tutafanya kila kitu kulinda jamii zetu.”
Ameongeza kuwa Israel tayari imefanya mashambulizi dhidi ya uwepo wa Uturuki na kuharibu uwezo wa kijeshi wa Syria, akisema Israel haitaruhusu Ankara “kuanzisha ngome” au ushawishi wa kijeshi nchini humo.
“Tulishambulia uwepo wa Uturuki na kuharibu uwezo wa Syria, na hatutaruhusu Uturuki kupata nafasi ya kujikita hapa,” alisema Katz.
Kauli ya Katz inaongeza mvutano kati ya Israel na Uturuki, ambazo tayari zimekuwa na tofauti kubwa kuhusu vita vya Gaza, sera za Mashariki ya Kati na ushawishi wa kijeshi katika eneo hilo.
Wachambuzi wanaonya kuwa ushindani wa ushawishi kati ya mataifa hayo mawili unaweza kuwa changamoto mpya katika mustakabali wa Syria na usalama wa Mashariki ya Kati.